Monday, January 31, 2011

Mjadala wa Katiba mpya hautazimwa

 Prof. Issa Shivji

 Jenerali Ulimwengu

 Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa

HAMISI KIBARI

MWANZONI mwa wiki hii, gazeti moja limemkariri Mbunge wa Monduli, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, akitoa tahadhari kwamba mjadala kuhusu Katiba mpya usiwe chanzo cha kuharibu amani iliyoko nchini. 

Kwa mujibu wa gazeti moja litokalo kila siku, Lowassa alisema kwamba kadri siku zinavyozidi kusonga mbele ndivyo eti moyo wa kuharibika kwa amani unavyozidi kuongezeka nchini.
Akakaririwa akisema kwamba eti  katika mijadala mbalimbali inayoendelea nchini, hasa ya Katiba, wananchi wanatakiwa kupingana kwa hoja na si kwa kuhatarisha amani.
Lowassa pia aliwashauri waimbaji wa Injili kutunga nyimbo zinazohamasisha na kuchochea utunzaji wa amani, ili iendelee kudumu. 

 “Hakikisheni mnatunga nyimbo za kutetea amani maana kwa sasa kila mtu ana lake analosema, vyombo vya habari vinachochea kwa njia yake, hivyo tuilinde hii amani,” alikaririwa akisema sentensi hiyo.

Ni kweli, tunahitaji kuona watu wakikemea mambo ambayo yanaweza kuhatarisha kuvunjika kwa amani tunayojivunia. Lakini swali la kujiuliza hapa ni hili; kweli mjadala kuhusu katiba mpya unaoendelea nchini kote, kuanzia kwenye majukwaa ya siasa, makanisani na misikitini hadi kwenye vijiwe vya kahawa una dalili yoyote ya kuvunja amani ama ni kuiokoa Tanzania isielekee kwenye kuvunjika kwa amani kama ilivyotokea kwa majirani zatu wa Kenya

Tunaambiwa kwamba  Lowassa alitoa (tahadhari?) hii wakati akifungua Studio ya muziki iiitwayo FLEM ya jijijini Dar es Salaam, lakini mimi ninajiuliza tena swali hili; Waziri Mkuu huyu wa zamani alikosa la kusema siku hiyo?

Lowassa alitoa kauli hiyo ikiwa ni siku takriban moja baada ya wanazuoni, wanasiasa na wanaharakati kukutana chuo kikuu cha Dar es Salaam kujadili na kupendekeza namna mchakato wa kuandika Katiba mpya unavyopaswa kufanyika.

Tangu nisome habari hiyo, nimekuwa ninajiuliza maswali kadhaa bila majibu ikiwa ni pamoja na haya; Je, Lowassa ameona wapi mjadala huu ukiwa na dalilia za uvunjifu wa amani ama ni yeye anayepandikiza kitu kingine ambacho sisi wengine hatukioni? 

Je, yeye hajayaona maeneo yenye dalili za kuvunja amani ya nchi yetu ambako alitakiwa kuharakisha kutoa kauli kama hizi?

Ninasikia aliwahi kutoa ushauri ambao ungeweza kuepusha vurugu za Arusha kama ungefanyiwa kazi kwa kutaka pande zilizokuwa kwenye mzozo kukutana kabla ya kilichotokea, lakini baada ya vurugu kutokea na kusababisha mauaji amesema nini? Je, kwa nini asilingetumia jukwaa la FLEM kuwasuta hao walioshindwa kutumia ushauri wake ili kuzuia yaliyotokea badala ya kuamua ‘kuuza sura’ akiongea ‘pumba’.

Je, wakati ule Tume ya Uchaguzi ya Taifa ilipokuwa inachelewesha kutoa matokeo huku ukweli ukiwa umeshabainika mshindi ni nani katika majimbo kwa sababu kura zilikuwa zinabandikwa kila kituo, alikuwa wapi kutoa kauli za kukemea hali kama hiyo kwa sababu inahatarisha amani ya nchi?

Ninachojua mimi, kama nitakavyoeleza hapa chini, wanaojadili umuhimu wa kuandikwa kwa Katiba mpya sasa ndio wanaoitakia mema nchi yetu iondokane na kuvunjika kwa amani siku moja. Hawa ni kuanzia watu wenye heshima katika jamii yetu kwa kufanya kazi zilizotukuka kama vile Jaji mstaafu Dk. Robert Kisanga, Jaji Mark Bomani, Profesa Issa Shivji, Jenerali Ulimwengu, Mwanasheria Mabere Marando, Dk. Benson Bana na wengineo.

Je, ni kweli Lowassa hajui kwamba msingi mkuu wa kilichotokea Kenya baada ya uchaguzi wa mwaka 2007 na kusababisha muaji ya takriban watu 1000 na wengine zaidi ya laki sita kukimbia makazi yao ni ubovu wa katiba? Je, hajui kwamba baada ya Kenya kuja na katiba mpya sababu zilizosababisha mauaji ya Kenya na ambazo zinaweza kutokea hapa kwetu wao wameondokana nazo?

Kwa kifupi ni kwamba sisi Tanzania tumeendelea kuwa na Tume isiyoonekana kuaminika na pande zote mbili, chama tawala na upinzani huku pia Katiba ikiwa hairuhusu kupinga uchaguzi wa rais wa mahakamani baada ya kutangazwa. Je, kadri wananchi wanavyozidi kujua haki zao hilo pekee la kutohoji uhalali wa kura za rais haliwezi kutupeleka pabaya siku moja?

Mimi nadhani Lowassa alipaswa kuwahamasisha makada wenzake katika CCM kuchangamkia mjadala wa uandikwaji wa katiba mpya kama anaitakia mema nchi yetu hata kama anadhani katiba iliyopo sasa inawabeba CCM kwa vile bado imejengwa katika mfumo wa chama kimoja.
Ninasema hivyo nikiwa nina habari kwamba wabunge na viongozi wengine wa chama tawala hatukuwaona katika kongamano lile la chuo kikuu kuhusu Katiba Mpya lililotayarishwa na Jumuiya ya wanataaluma wa chuo hicho (Udasa).

Hebu tuangalie kwa kifupi yaliyojiri kwenye kongamano hilo la Jumamosi iliyopita kama kweli yaneweza kuhatarisha amani ama kusaidia kuijenga: Profesa Issa Shivji ambaye alikuwa mmoja wa watoa mada, alisema kwamba wakati sasa umefika kwa wananchi wa Tanzania kuwa na katiba mpya ambayo itajumuisha misingi ya taifa itakayokuwa imelinda maslahi ya wananchi.
Tena akasema suala hilo lisiachwe kwa wanasiasa (kama Lowassa)  kwani katiba mpya inapaswa iangalie maslahi ya walio wengi na hasa wanaoishi vijijini kwa kuangalia ardhi, madini, wanyama na maliasili nyingine. Pia alisema  Katiba hiyo inapaswa kuangalia mfumo mzima wa serikali kwa ajili ya kuboresha maisha ya wananchi.
Je, mjadala kama huo ambao  Jenerali Ulimwengu, alisema wakati umefika kwa wananchi kushiriki moja kwa moja kwenye mchakato wa kuandika katiba mpya kwa kuwa historia inaonyesha kwamba mabadiliko ya katiba yaliyofanywa huko nyuma hawakushirikishwa unavujanje amani kwa mujibu wa mtazamo wa Lowassa?
Hata mimi ninakubaliana na Jenerali alivyosema; “Wakati umefika kwa raia kuwa na nafasi juu ya serikali yao na siyo serikali kuwa na nafasi juu ya wananchi. Ni fursa ya kujiangalia upya na tusikubali kwenda haraka haraka; si zoezi la Rais, Bunge, vyama vya siasa, wanazuoni au waandishi wa habari, ni la Watanzania wote.”
Hivi Lowassa angetaka mjadala wa katiba mpya ufanywe na akina nani ili aone kwamba hakuna uvujifu wa amani… Makada wa CCM ambao wanakimbia maeneo kama haya? 
Kweli mtu kama Lowassa anaweza kukubaliana na pendekezo alilolitoa Jenerali kwamba mjadala kuhusu mchakato wa katiba mpya uanze ndani ya vyama vya kiraia, kuona namna ya kuboresha misingi itakayolinda masilahi ya wananchi ili wawe na usemi kuhusu raslimali zao na serikali yao
Lowassa huyu tunayemfahamu, ambaye hakuachia ngazi ya nafasi ya Uwaziri Mkuu kwa moyo mmoja inatia shaka kama anaweza kufurahia ushauri kama huu ulioendelea kutolewa na Jnerali Ulimwengu katika kongamano hilo kwamba mchakato wa kuandika Katiba mpya utaisaidia Tanzania kujisanifu upya kwa kutambua rasilimali zote za taifa zilizo chini na juu ya ardhi na kuainisha umiliki na matumizi yake.
Jenerali alisema kwa usanifu huo, taifa litaweka bayana nani mwenye mamlaka ya kuruhusu matumizi ya rasilimali hizo na kwa wakati gani kuliko ilivyo katika katiba ya sasa.
Mimi binafsi, ninaaamini kama alivyosema mbunge wa Iramba Mashariki (Chadema), Tundu Lissu, kwenye kongamano hilo kwamba katiba iliyopo hivi sasa haiwezi tena kutumika kwa kuwa ina makosa mengi ambayo hayawezi kuendelea kuvumiliwa.
Ninaamini hata Lowassa anajua kwamba jambo moja kubwa ambalo haliwezi kuendelea kuvumilika ni katiba hii kuendelea kukibeba chama tawala, katika mfumo huu wa vyama vingi unaoruhusiwa na katiba hiyo hiyo. Mambo mengine ni Rais kuendelea kuwa na madaraka makubwa huku wananchi wakiwa hawana uwezo wa kuamua na kuhoji kuhusu matumizi ya raslimali zao (hata kama ni kwa kupitia wawakilishi wao, yaani wabunge).
Ninamtaka pia Lowassa ajue kwamba sisi wananchi tunaojadili katiba mpya katika kipindi hiki cha amani badala ya kusbiri mambo yaharabike kama ilivyotokea Kenya tunaamini kwamba tumaini letu kubwa katika kulinda uhuru wetu na kushuhudia anguko la mafisadi na viongozi wasiofaa ni katiba mpya.
Wananchi tumechoka kuendelea kuona watu wachafu wakinunua uongozi na kusimama kwenye majukwaa wakipigiwa makofi badala ya kuwa jela kutokana na kuwaibia Watanzania raslimali zao kila kukicha.
Wananchi tumechoka na watu waliogeuza siasa kuwa mradi mkubwa wa kuwatajirisha wao na familia zao kwa njia za mkato na kuuacha umma mkubwa wa Watanzania ukitopea katika lindi la umaskini.
Na nionavyo mimi, moto wa mageuzi ya katiba hauwezi kuzimwa na kauli rejareja kama hizi za Lowassa ama wengine wenye matazamo kama wake.
Kadhalika, nionavyo mimi Watanzania kwa asili yao ama walivyojengwa na tawala zilizopita, hususan enzi za Mwalimu Julius Nyerere ni wapenda amani na ndio mana wamekuwa wakifumbia madudu mengi sana kama vile hawaoni likiwemo la kunyimwa haki ya kupinga uchaguzi wa rais mahakamani. Yapo mambo yanayowakera sana watanzania, kubwa likiwa ni ufisadi unaosababisha raslimali zao kuporwa na wajanja wachache. Kama ndivyo, na kama ana ubavu, hayo ndiyo mambo ambayo Lowassa alitakiwa kuwaambia waimba Injili watunge nyimbo za kuyakemea badala ya kuwataka eti kukemea amani ambayo tunayo na halijawa tatizo kiasi hicho. Au Lowassa hana ubavu (moral authority) wa kuwataka waimba Injili sasa kulipuka na nyimbo kila kona wakikemea ufisadi?!!
Lowassa pia amevihusisha vyombo vya habari kwa kudai kuchochea kuvurugika kwa amani kupitia mjadala wa katiba kitu ambacho pia kinashangaza. Ninavyojua mimi vyombo vingi vya habari, ukiachilia mbali vya marafiki zake wanaomuunga mkono, vinapigania maslahi ya nchi ambayo pengine kwa Lowassa anaona kama ni kuvuruga amani. Vyombo vya habari likiwemo gazeti hili vimejitahidi kuonyesha uzalendo wa kweli kwa nchi yetu.
Vyombo vya habari vinavyotetea mafisadi na ufisadi, kama anaweza, ndivyo alivyopaswa kuvinyooshea kidole kwanza na hivi ndivo, kwa mtazamo wangu, vinavyokejeli mijadala yenye manufaa kwa nchi yetu.

Mwandishi ni Mhariri wa gazeti hili. Unaweza kuwasiliana naye kupitia  Email: hkibari1965@gmail.com au simu 0713328006/0758 143457/ 0789328006