Thursday, August 25, 2011

Tusifananishe ya Libya na yaliyojiri Misri, Tunisia

 

HAMISI KIBARI
Dar es Salaam

Kanali Muammar Gddafi
WAKATI niliposikia maandamano yameibuka nchini Libya ya kutaka kumuondoa madarakani Kanali Muammar Gadaffi aliyetawala nchi hiyo kwa miaka 42, niliunganisha na yale yaliyoziangusha serikali za Misri na Tunisia.
Kama walivyo Watanzania wengi, nilichukulia kwamba ni wimbi la mageuzi yanayotokana na nguvu ya umma katika nchi za Kiarabu baada ya watawala wake kung’ang’ania madaraka kwa muda mrefu. Nchi nyingine za Kiarabu zinazokumbwa na machafuko ni Yemen, Bahrain na Syria.
Kama walivyo wapenda demokrasia wengi duniani, hakuna anayependa kuona mtu mmoja anataka kutawala milele na huku akiandaa wanawe kumrithi na kutaka kujenga utawala wa kifalme. Kwa msingi huo, nilianza kuunga mkono juhudi za kumng’oa Gadaffi madarakani.
Lakini kadri siku zilivyokwenda, taratibu nilianza kushituka. Niligundua kwamba yanayotokea Libya si mapambano ya nguvu ya umma, bali kuna uasi. Yaani wale wanaoandamana wanatumia silaha za moto kutaka kumng’oa madarakani Gadaffi tofauti na tulivyokuwa tunaaminishwa, na hususan kupitia vyombo vya habari vya Magharibi.
Nilitilia shaka zaidi hali inayotokea Libya kutokana na waasi kuungwa mkono na ubeberu wa nchi za Magharibi ukiongozwa na Marekani.
Mwanzoni tulisikia kutolewa kwa Azimio la Umoja wa Mataifa (UN) lililodai kwamba Umoja wa Kujihami wa nchi za Magharibi (Nato) sambamba na Marekani wanaanzisha operesheni tu ya kibinadamu nchini Libya. Yaani tulichoaminishwa kujua ni kwamba majeshi ya Gaddafi yanakiuka haki za msingi za raia ikiwa ni pamoja na kuua watu na hivyo Nato ilikuwa inaingia pale kwa lengo la kuwahami wananchi wasio na silaha dhidi ya utawala dhalimu.
Lakini kilichokuja kujitokeza baadaye ni kwamba mapigano yale nchini Libya ni ya Nato kwa mgongo wa waasi, yakiwa na lengo la kubadilisha uongozi na si kuwahami raia.
Kingine kinachotia kichefuchefu ni Nato kutotaka kusikiliza ushauri wa viongozi wa Umoja wa Afrika (AU) ambao ulionekana ukitafuta suluhu bila kumwaga damu zaidi lakini Nato haikutaka kuwasililiza. Na hii kwa kweli ni udhalilishaji wa viongozi wetu wa Afrika.
Kadhalika, Gaddafi aliwahi kukaririwa kutaka mazungumzo na waasi katika kuamua mustakabali wa nchi hiyo, lakini waasi walikataa katakata. Nia yao ni lazima Gaddafi aondoke, si kwa sanduku la kura bali kwa mtutu.

Nilibahatika kuongea na kijana mmoja Raia wa Libya anayesoma Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam akanisimulia kwa kifupi mtazamo wake na mapigamo katika nchi yao. Yeye anamuunga mkono Gaddafi na alijibu maswali yangu na wengine tuliokuwepo tukimsikiliza. Kwa kweli kijana huyu wa Libya, ameongeza mtazamo wangu kuwa hasi zaidi dhidi ya ubeberu unaofanywa na nchi za Magharibi na Marekani dhidi ya Afrika. Kiasi kwamba ninawaomba wachambuzi wenzangu wakati tunapoliangalia suala la Libya, tujue pia kwamba hapa kuna ubeberu: Maswali yetu dhidi ya kijana huyu kutoka Libya aliyeko Tanzania na ambaye anamuunga mkono Gaddafi yalikuwa namna hii:
SWALI: Kwa nini unawapinga waasi?
YEYE: Unajua waasi asili yao wanatokea katika mjini wa Benghazi. Hapa ni kwao aliyekuwa kiongozi wa Libya aliyepinduliwa na Gaddafi. Siku zote watu wa Benghazi wamekuwa hawaridhiki na utawala wa Gaddafi, siyo kwamba hauna mafanikio bali ni kwa sababu wanaamini kwamba lazima wao ndio watawale Libya. Kwa hiyo utaona kwamba hawapigani si kwa sababu nyingine isipokuwa uroho tu wa madaraka.
SWALI: Lakini Gaddafi analaumiwa kwa udikteta na kutaka kufia madarakani, kwa maana kwamba haruhusu demokrasia ishamiri nchini Libya. Unasemaje?
YEYE: Huo ndio mtazamo wa wengi hasa huku Tanzania na kwingineko. Mbaya zaidi wengi mnalishwa taarifa za Kimagharibi ambazo hazina ukweli wowote. Lakini ninachojua mimi Gaddafi si rais na wala haongozi nchi kibabe. Katika nchi yetu ameruhusu watu kushiriki katika mabaraza na kuamua mustakabali wa mambo yao na yeye haingilii kati. Wananchi wakiamua kwamba Waziri fulani hafai ama ameshindwa kutekeleza hili ama lile lazima aondoke madarakani, si kama hapa Tanzania nimeona waziri si rahisi kuondolewa madarakani kwa nguvu ya wananchi.
SWALI: Kwa hiyo wewe ungependa Gaddafi aendelee kutawala milele?
YEYE: Sina jibu la moja kwa moja lakini ukweli ni kwamba Gaddafi ametufanyia mengi watu wa Libya ambayo ninaamini hakuna mtawala atakayeweza kufikia alikofika.
Unajua nchi yetu ni Jangwa, na ukisikia maisha yalivyokuwa kabla ya kuja kwa Gaddafi madarakani utashangaa sana. Kulikuwa na umaskini wa kutisha. Lakini serikali ya Gaddafi ni serikali inayowajali wananchi kuliko serikali yoyote duniani ambayo mimi ninaifahamu. Kwanza katika nchi yetu, licha ya kuwa ni jangwa, hakuna taabu ya maji kama hapa Tanzania, mkate ni bei rahisi sana kama shilingi 250 tu ya Tanzania, sukari ni rahisi, elimu na matibabu ni bure. Watu wanaotaka kuoa na hawana uwezo wanalipiwa na serikali mahari na kupatiwa msingi wa maisha. Watoto wote yatima ni mali ya serikali. Si rahisi kuona chokoraa (watoto wa mitaani) kama huku kwenu Tanzania.
SWALI: Lakini, pamoja na kufanya yote hayo,  Gaddafi anadaiwa kujilimbikizia mali kibao nje ya nchi. Unasemaje kuhusu hilo?
YEYE: Mimi ninadhani ni propaganda tu za Kimagharibi. Ninaamini hizo ni pesa za serikali zinatokana na mafuta. Kwa sababu mafuta hayauzwi kama kanzu dukani, kwamba ukiuza unalipwa hapo hapo. Mimi ninaweza kusema hata kama Gaddafi amejitunzia mapesa huko nje, wacha ajitunzie kwa sababu wakati anaingia madarakani hakukuta kitu lakini kasimamia uchumi vizuri kiasi kwamba hatuombiombi nje kama wengine na hakuna mwananchi anayelalamika kwamba serikali imeshindwa kufanya hili ama lile.
Ninaweza kusema Libya kama hakuna mikataba mibovu kama ninayosikia katika nchi nyingine ikiwemo hapa Tanzania. Raslimali zetu tunazifaidi Walibya. Mimi ninaamini hili linawaudhi sana mabeberu wa Magharibi ambao wanapenda sana kutunyonya Waafrika.
Kinachowasumbua waasi ni chuki tu kwa sababu wanaamini kwamba mtawala lazima atoke Benghazi na siyo Tripoli.
SWALI: Lakini tunaona waasi wakishangiliwa na wananchi kwa kukomboa maeneo. Unasemaje?
YEYE: Kwanza usiite kukomboa bali ni kuyateka. Kinachofanyika ni propaganda tu za vyombo vya habari vya Magharibi. Mimi ninawasiliana na marafiki zangu, ndugu zangu karibu kila sehemu nyumbani Libya, lakini wote hawaonekani kuwaunga mkono waasi. Kile kinachofanyika ni kwamba waasi wanapiga sehemu, hata kama ni mbali na mji, kisha wanaita waandishi wao na kutangaza kile ambacho ulimwengu unatakiwa kujua na si ukweli halisi wa mambo. Yaani kwa kweli ukisoma habari za vyombo vya Magharibi na kusikia wananchi wanavyosema ni vitu viwili tofauti. Nyinyi hamwezi kuona uongo wa waasi walivyodai majuzi kwamba wamewateka watoto wa Gaddafi lakini baada ya muda ikagundulika kwamba ni uongo mtupu.
Ninachoweza kusema ni kwamba kinachotuponza Libya ni msimamo wa Gaddafi wa kupinga unyonyaji wa Magharibi. Wanachotafuta kwetu ni mafuta yetu basi. Kwa nini hamjiulizi kwamba Nato hawakupeleka majeshi Misri, Syria wala Tunisia? Kwa mfano wanadai Gaddafi anaua raia kwani hamjui Hosni Mubaraka wa Misri anashitakiwa kwa serikali yake kuwashambulia waandamanaji waliokuwa wakimpinga? Mbona Nato hawakupeleka majeshi? Je, mnasemaje kuhusu Syria, mbona hakuna majeshi ya Nato? Yaani tunadanganywa sana Waafrika.
SWALI: Unazungumziaje majaaliwa ya Libya?
YEYE: Ninajua mpaka sasa wanapiga sana Tripoli lakini majeshi ya Gaddafi bado yako imara. Lakini lolote linaweza kutokea lakini ninajua si muda mrefu Walibya tutaikumbuka neema ya Gaddafi. Mimi ninaombea ushindi kwa Gaddafi.

No comments:

Post a Comment